27 May 2006

Graca Simbine Machel.


Kuna nchi nyingi sana za Afrika ambazo unaweza kuzungumzia historia zake bila kutaja wake wa viongozi waasisi wa mataifa hayo na bado historia ikakamilika. Kwa nchi ya Msumbiji kitu hicho hakipo!. Hauwezi kuelezea historia ya Msumbiji bila kumuhusisha bibi Graca Machel ambaye ni mjane wa Rais wa kwanza wa Msumbiji Ndugu Samora Machel(Mzee wa kombati)

Graca Simbine ni mwanamke mwenye hulka ya upole lakini ni mwenye akili nyingi na makini sana katika utekelezaji wa mambo yake. Ni mtu asiyekurupuka wala kuyumbishwa na mikumbo ya kijamii. Kwa ufupi ni mtu anayefanya jambo kutokana na imani yake inavyomuongoza.

Mwanamke huyu wa shoka alizaliwa tarehe 17-10-1946 katika eneo la pwani ya ukanda wa Gaza nchini Msumbiji. Akiwa ni mtoto wa mwisho kati ya watoto sita wa mzee Simbine na bibi Nelly ni yeye peke yake ambaye hakubahatika kumuona baba yake kwani alizaliwa majuma matatu baada ya baba yake kufariki. Mzee Simbine ambaye alikuwa akifanya kazi katika misheni ya Methodist hapo kijijini, aliacha maagizo kabla ya kufa kwake kwamba mkewe na watoto wake wakubwa ni lazima wahakikishe mdogo wao (Graca) anakwenda shule hadi masomo ya juu. Alipofikisha miaka 6, dada yake mkubwa aliyekuwa mwalimu alimchukua na kumuingiza shule, anasema dada yake alikuwa ni kama mama yake wa pili kwa jinsi alivyomlea vizuri na kuhakikisha anafanya vizuri katika masomo yake, na kutokana na usimamizi mzuri wa dada yake aliweza kufaulu masomo yake ya msingi na kupewa nafasi na misheni ya Methodist kwenda kusoma sekondari. Anasema akiwa sekondari ndipo alipoanza kubaini ubaguzi uliopo kati ya weusi na weupe kwani darasani kwao alikuwa mweusi peke yake kwa hiyo aliona jinsi alivyokuwa akibaguliwa na kutengwa na weupe. Lakini kama nilivyosema hapo awali kwamba yeye si mtu wa kuyumbishwa hilo la kubaguliwa halikumfanya kushindwa kuzingatia masomo yake na mara nyingi anasema jambo moja lilikuwa likimfariji kwamba hata kama alikuwa akibaguliwa lakini alijua Msumbiji ni ya kwake na si yao na wao wako kwake, hivyo alifanya masomo yake vizuri na kufanikiwa kupata tena ufadhili wa kwenda chuo kikuu cha Lisbon Ureno kusomea Lugha hiyo ilikuwa mwaka 1968.

Akiwa Lisbon alikutana na watu wengi wenye fikra mbalimbali za kimapinduzi, akasikia pia habari za FRELIMO chama ambacho kilikuwa kinapigania ukombozi wa Msumbiji. Graca akajiunga kwa siri katika chama cha FRELIMO, lakini haikupita muda mrefu serikali ya kikoloni ikagundua anachokifanya Graca na hivyo ikaandaa adhabu ya kwenda gerezani pindi Graca atakaporejea Msumbiji. Graca kwa kulijua hilo ikabidi asimalize masomo yake na kukimbilia nchini Uswisi. Mwaka 1973 akiwa bado ulaya akaamua kujiweka wazi kama mwanasiasa na mpigania uhuru wa nchi yake na mwaka uliofuata 1974 chama cha FRELIMO kilimrudisha Afrika lakini nchini Tanzania ambapo ilimpatia kazi ya kuwa mkuu wa shule ya sekondari ya FRELIMO iliyokuwa Bagamoyo, shule hii siku hizi hujulikana kama shule ya sekondari ya Kaole. Chama cha FRELIMO kilikuwa na shule nyingi za sekondari katika nchi huru za Afrika nia ikiwa ni kuwapatia elimu wananchi wake huku harakati za ukombozi zikiendelea. Akiwa Tanzania alijifunza pia mafunzo ya kijeshi ya kujilinda na ni katika kipindi hiki ndipo alipoweza kukutana na mzee wa kombati Samora Machel. Graca na Samora walianza kama marafiki wa kawaida lakini baadaye urafiki ukazidi na kuwa wapenzi wakati huo ikiwa ni miaka mitatu tu imepita tangu Samora afiwe na mkewe wa kwanza Josina Machel.

Harakati za FRELIMO ziliendelea vizuri kwani mwaka uliofuatia tarehe 25-06-1975 Msumbiji ilijipatia uhuru wake kutoka wa Wareno, mwaka huo huo Graca alifunga ndoa na Samora machel.

Kutokana na elimu yake na uzoefu wake wa kufundisha, na jinsi alivyoweza kuishika vizuri nafasi ya ukuu wa shule ya FRELIMO Bagamoyo, serikali mpya ya Msumbiji iliona haina sababu kumnyima Graca nafasi ya uwaziri wa elimu na utamaduni. Akiwa wanamke pekee na wa kwanza kushika nafasi hiyo kubwa anasema kwanza alipigwa na butwaa na kutetemeka hakujua kama ataweza kuimudu au la!...alijifungia siku kadhaa chumbani kwake akili na kujiuliza kama akikataa si ataonekana mdhaifu? na je akikubali halafu asiimudu si watasema '..unaona matatizo ya kuwapa nafasi wanawake..!!' Lakini baada ya kujufikiria kwa muda alifuta machozi na kuchukua kazi!! Lengo lake likiwa moja, kuhakikisha watoto wote wa Msumbiji wanakwenda shule. Kwa mafanikio makubwa alibadilisha kabisa hali ya elimu ya Msumbiji kiwango cha watoto kwenda shule kiliongezeka mara dufu kutoka watoto 400,000 aliowakuta alipoishika wizara hadi 1,500,000 ikiwa ni asilimia 72 zaidi.

Haya popote penye maendeleo adui hakosi kujitokeza, mwaka 1976 kikundi kidogo cha wananchi wa Msumbiji wakaunda chama cha kuipinga Frelimo kilichojulikana kama RENAMO. Chama hiki kilikuwa kikifadhiliwa na wazungu kutoka Rhodesia(Zimbambwe), Afrika ya kusini na Marekani. Wazungu hawa waliunda na kufadhili RENAMO ili kuiadhibu Msumbiji kwa kuisaidia makazi wafuasi wa ANC. Kazi ya kikundi hiki cha RENAMO ilikuwa ni kufanya uharibifu katika sehemu zote za maendeleo ambapo FRELIMO ilikuwa ikifanya mfano, ilibomoa mashule na hospitali zilizojengwa na FRELIMO, iliharibu reli na mengine mengi, jambo hili lilimtingisha sana Graca ukizingatia wizara yake nayo ilikuwa ni kati ya tageti za RENAMO. Mwaka 1984 Samora Machel alikubali kusaini mkataba na wafadhili RENAMO wa makubaliano ya kuacha kuifadhili RENAMO na FRELIMO kuacha kuipa msaada wa makazi wafuasi wa ANC. Inasemeka kwamba kwa Samora kusaini mkataba ule ni kama alikuwa akisaini mkataba wa kifo chake, kwani miaka miwili baadaye tarehe 19-10-1986 alifariki katika ajali ya ndege inayosemekana ilipangwa na hao hao wazungu wa Afrika ya kusini. Samora alikuwa akirudi nyumbani kutoka katika mkutano Lusaka Zambia.

Kifo hiki kwa Graca kilikuwa ni pigo kubwa sana. Hakuamini ilikuwa ni ajali ya kawaida alijua na alisema waliomuua mume wangu ndiyo walewale waliomfunga Nelson Mandela. Maneno haya alimuandikia Winnie Mandela wakati wa msiba kwamba "wanadhani kwa kukata miti mirefu zaidi katika msitu watakuwa wameteketeza msitu wote!! ni wale wale waliomuua mume wangu ndiyo waliomfunga mume wako.."

Kwa miaka mitano mfululizo tangu Samora Macheli afariki, Graca alivaa nguo nyeusi peke yake. Na ilipofika mwaka 1989 alistaafu wadhifa wake wa uwaziri na kujishughulisha na shughuli za maendeleo ya jamii hasa hasa watoto. Mungu si Athumani Mola akaona si vyema Graca kuendelea kuishi peke yake hivyo akamtafutia mwenzi mwingine ambaye pia ni shujaa wa Afrika Bwana Nelson Mandela. Mwaka 1998 Graca alifunga pingu za maisha kwa mara ya pili na Mandela ambaye alitengana na mkewe Winnie Mandela mwaka 1992. Winnie anadai iko siku ataongea juu ya mahusiano ya watu hawa wawili.

Graca alibarikiwa kupata watoto 7, ambapo wawili ni wa kuzaa mwenyewe na watano ni wa wake wawili wa kwanza wa Samora. Hadi leo hii Graca ameweka rekodi ya kuolewa mara mbili na marais wawili mashujaa wa nchi tofauti tena katika ndoa zote akiwa ni mke wa tatu.

08 May 2006

Da' Mija na wanawake wa shoka yafunga mwaka!!

Shukrani hoi hoi na vifijo vimuendeee ndugu Ndesanjo Macha popote pale alipo kwani kama si yeye leo hii nisingekuwa naandika haya ninayo yaandika. Ndesanjo ndiye aliyenikurupua huko nilikokuwa na kusisitiza kwamba ni lazima nifungue blogu, nilikwepa kwepa lakini wapi jamaa alikuwa na mimi tu mwishowe nikaona ngoja nikate shauri na leo hii nayaona matunda yake. Sio siri ufahamu wangu sasa umeongezeka-ongezeka.

Labda niwapeni kisa kizima cha Ndesanjo kunibabatiza. Nilikuwa katika harakati zangu mtandaoni mara nikakutana na blogu ya Jikomboe, kuangalia vizuri naona Ndesanjo Macha..nikajiuliza huyu mtu huwa namsikia sikia ngoja nione anafanya nini na humu mtandaoni, basi nikaanza kumfuatilia na kwa kweli makala zake zilinitia nguvu sana nikajisemea peke yangu..'haiwezekani huyu mtu lazima nimjue zaidi'.. basi siku moja nikaona nimtupie kaji-swali ambako kanaonyesha niko kinyume na yeye yaani kama mpinzani wake nione atajibu nini!.. mara nyingi mimi nikiona mtu anafanya vitu vizuri hupenda kujua na anapokoselewa hupokeaje hali hiyo? Wee! nilipata jibu hilo mwenyewe nilitulia bahati mbaya nimesahau hata jibu lenyewe labda kama Ndesanjo unalikumbuka. Basi kuanzia hapo Ndesanjo akajua huyu mtu yuko kinyume na mimi kwa hiyo akawa amekaa mkao tayari tayari, mimi sina hili wala lile siku moja nikatoa maoni katika habari fulani ya "Nimtume nani" nikamwambia labda umetumwa wewe kwani Mungu haangalii mtu fulani ili kumtuma". Sasa hapa nikamchanganya kidogo kwamba huyu Da'Mija yuko upande upi? yuko upande wangu au ananidhihaki?... akanipiga swali Kwani wewe kwako Mungu ni nini au ni kitu gani?? Duh! nikaona haya tena mengine...kaka yangu hapa hakunielewa lakini na mimi sikufanya ajizi nikamuelewesha Mungu ni nini, ni nani kwa jinsi nilivyokuwa nikimuelewa. Baada ya maelezo hayo ndiyo akasema wewe binti ni lazima ufungue blogu yako. Basi nikaona huyu Ndesanjo lazima atakuwa ametumwa na kwangu mimi pia. Hivyo nikafungua blogu yangu. Hadi sasa hivi ingawa sina data kamili, lakini ninaamini huyu bwana ndiyo ameweza kushawishi watu wengi zaidi kufungua blogu zao. Ubarikiwe Ndesanjo, tubarikiwe wanablogu wote.

04 May 2006

Boyz 11 men sasa kiboko!!


Haya tena, ahadi ndio zinazidi kumiminwa na uongozi wa awamu ya nne. Hivi majuzi wakati wa sherehe za mei mosi ambapo kitaifa zilifanyikia Shinyanga Ndugu rais ameahidi kushughulikia suala zima la mishahara, sasa sijui ni ya kweli au la! na ni kwa kiwango gani itaongezwa bado sina hakika.. MtiMkubwa kaniletea hii habari hapa ili wote tushuhudie hizi ahadi. Soma habari yenyewe hapo chini...



2006-05-02 16:53:55
Na Mwandishi Wetu, Jijini

Rais Jakaya Kikwete na Waziri wake Mkuu, Bwana Edward Lowassa, marafiki ambao watoto wa mjini waliwahi kuwaita Boyz ll men, wamewadhihirishia Watanzania kwamba hawana mchezo na wamepania kuboresha hali za Watanzania.

Rais Kikwete alidhihirisha hilo jana wakati anahutubia mamia ya wananchi katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, Mei Mosi, Rais Kikwete, sherehe zilizofanyika kitaifa mkoani Shinyanga katika uwanja wa Kambarage.

Katika hali ambayo inaonyesha Rais amepania kutofanya mambo ya danganya toto katika uongezaji wa mishahara na kuboresha maslahi ya watumishi, alitangaza mikakati kadhaa.

Mosi: Alisema ataunda tume itakayotoa hali halisi ya maslahi ya watumishi iliyopo Serikalini na kwenye mashirika ya umma.

Rais alisema tume hiyo pamoja na mambo mengine, itashughulikia uchambuzi wa mishahara na maslahi ya watumishi hao.

Kwa mtaji huo, ’watemi’ Serikalini na katika mashirika ya umma ambao siku zote wanapigania kuongezwa kwa maslahi yao wenyewe, sasa wataumbuka.
Pia madaraja makubwa ya watumishi walionacho na akina pangu pakavu tia mchuzi, yataondoka.

Na kwa upande mwingine, watumishi wasio na nafasi ambao hali zao zimedhoofu kutokana na maslahi duni, watatamba katika uwanja wa haki na usawa.

Rais Kikwete alisema tume hiyo ataitangaza rasmi wiki ijayo na anataka kabla ya mwaka huu kuisha iwe imemaliza kazi hiyo.

Alisema mara baada ya Tume kumaliza kazi na kumpa mapendekezo, hataweka usiku na badala yake atayashughulikia mara moja na kutoa uamuzi juu ya hatua za kuchukua.

Pili: Rais ametaka Mabaraza ya Kisekta ya mishahara ya Kima cha Chini cha mishahara yaundwe mengi ili kushughulikia maslahi ya kundi hilo.

Kwa mtaji huo, kilio cha muda mrefu cha walalahoi huenda kikapungua.
Kwa muda mrefu, wafanyakazi wa kima cha chini wamekuwa wakilalamika kwamba ’wako jangwani’ kutokana na maslahi duni.

Tatu: Rais alisema suala la ajira amelishikia bango na kwamba mikakati inakamilishwa na muda si mrefu Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana italifahamisha Taifa.

Alisema dhamira ya Serikali ni kuongeza ajira kwa Watanzania na kwamba imedhamiria kuweka mazingira mazuri ambayo yatawezesha kukuza ajira nchini ili Watanzania wanufaike na kupunguza dhiki ya maisha.

Nne: Rais pia alizungumzia suala la kuajiriwa kwa wageni katika nafasi ambazo zingeweza kufanywa na Watanzania.

Alisema Serikali itakuwa makini na yenye ukali kwa ajira za aina hiyo.
Kwa kauli hiyo, malalamiko yaliyozagaa kwamba kuna Ma TX feki wanafanya kazi ambazo hata Wabongo ambao hawakwenda shule wanaweza kuzifanya, yatapungua.

Wananchi mbalimbali walioongea na gazeti hili kuhusu hotuba ya Rais walisema serikali ya awamu hii ni kiboko na kama yote yaliyoahidiwa yatatekelezwa, hali za Watanzania zitainuka.